Wednesday 20 November 2013

Kwa nini Tanzania ikae daraja la tatu EAC?


Hivi karibuni Rais Jakaya Kikwete alitoa msimamo wa Tanzania kuhusu hali ya sintofahamu inayojitokeza katika Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC), kuwa haikusudii kujitoa wala kuwa sehemu ya lawama iwapo jumuiya hiyo itayumba au kuvunjika.
Msimamo wa Kikwete unatokana na hali ambayo imejitokeza kwa miezi kadhaa ambapo nchi za Kenya, Uganda na Rwanda zimekuwa zikikutana, kujadili na kuafikiana katika masuala yanayohusu EAC kama usafiri, visa, forodha na mengine yanayoaminika kuwa ni sehemu ya mambo yaliyokwishajadiliwa au kukubaliwa na EAC.
Hatua za nchi hizi zimezua hisia kwamba Tanzania na Budundi zimekuwa zikitengwa. Kabla ya Kikwete kutoa msimamo, suala hili liliibuliwa bungeni na Waziri wa  Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Samuel Sitta, akitoa msimamo wa awali wa serikali, kuhusu mshikamano wa nchi hizo tatu.
Si kusudi la makala haya kuchambua msimamo wa Tanzania kuhusu mgogoro huo, bali kuhoji kwa nini Tanzania, kama nchi, imeachia usukani wa Jumuiya ya Afrika Mashariki na si tu kujiweka katika kiti cha nyuma, bali kwenye daraja la tatu katika ‘basi linaloelekea kwenye Shirikisho la Afrika Mashariki?’
Kwa wale ambao wameshuhudia awamu zote nne za uongozi wa nchi hii watakuwa na faida ya kulinganisha jinsi serikali za awamu zote zilivyoshughulikia masuala mbalimbali, hasa kuhusu jirani zetu.
 Awamu ya Kwanza iliwajengea Watanzania moyo wa kujiamini. Walipambana vilivyo, kitaaluma na kiuweledi na wenzao wa Kenya na Uganda. Tanzania haikuwa na hofu juu ya nchi hizi. Kwa hakika ilikuwa ni mfano wa kuigwa kwa wapenda maendeleo wote ndani ya Kenya na Uganda, baadhi ambao walihitimu masomo katika Chuo Kikuu cha Dar es Salaam. Msingi huo wa kujiamini ulijengwa na viongozi wa awamu hiyo.
Tangu awamu hii ya nne ishike hatamu, tumeshuhudia viongozi wakiwatia hofu raia wa Tanzania kuhusu masuala ya ardhi na ajira. Eti tukifungua mipaka jirani zetu watafurika na kupora ardhi yetu. Eti ufunguaji wa mipaka yetu utawaleta jirani zetu kuzinyakua nafasi za ajira na vijana wetu kubaki bila kazi.
Haya yanasemwa na viongozi wetu wa ngazi za juu.  Kwanza, suala la ardhi limetiliwa chumvi sana na wanasiasa. Hakuna nchi yeyote ya Afrika Mashariki iliyo na sheria kali kuhusu umiliki wa ardhi kama Sheria ya Ardhi ya Tanzania. Kwa mujibu wa sheria hiyo mtu asiye raia hawezi si tu kumiliki ardhi, bali hata nyumba nchini Tanzania.
Hata wale tunaowaita wawekezaji wanamilikishwa ardhi kupitia Kituo cha Uwekezaji Tanzania (TIC) na miliki hiyo, hubaki mikononi mwa kituo. Kwa misingi hiyo, hata tukifungua mipaka, haitakuwa rahisi kwa mgeni kuja na kumiliki ardhi bila kufuata taratibu zilizowekwa kisheria.
Katika nchi jirani za   Kenya, Uganda na Rwanda, Mtanzania anaweza kwenda huko akanunua nyumba bila tatizo. Kwa mantiki hii, hofu zinazoenezwa na wanasiasa wetu hazina msingi.
Katika suala la ajira ni lazima tukiri kuwa viwango vya elimu nchini mwetu vimeshuka sana na hakuna juhudi zozote zinazoonekana kuibadilisha hali hii.
Nimesikia baadhi ya wawekezaji, hasa kwenye hoteli, wakilalamika kuwa vijana wa Kitanzania hawajui Kiingereza na pia ni rahisi kwao kuajiri vijana kutoka Kenya. Labda hali hii ya kuajiriwa kwa Wakenya katika sekta zetu inaweza kutugutua kutoka kwenye hali hii ya kuridhika na mfumo wa elimu yetu

No comments:

Post a Comment