Monday 12 January 2015

NHC Arusha kujenga nyumba 4,500.Drive Hot News


 Kisarika alisema katika ujenzi wa nyumba hizo, zitakuwapo za gharama nafuu 520 na kati ya hizo, 300 zitaanza kujengwa Machi mwaka huu.

Arusha. Shirika la Nyumba la Taifa (NHC) kwa kushirikiana na wadau mbalimbali wa Arusha, litajenga nyumba za kisasa 4,500.
Nyumba hizo za gharama nafuu, zinatarajiwa kujengwa katika Kata ya Mateves, wilayani Arumeru na Olasiti, Wilaya ya Arusha Mjini.
Akizungumza jana kwenye kikao cha Kamati ya Ushauri Arusha (RCC), Meneja wa NHC Arusha, James Kisarika alisema wamejiweka mkakati wa kuanzisha mji mpya utakaojulikana kama Safari Satellite.
Kisarika alisema katika ujenzi wa nyumba hizo, zitakuwapo za gharama nafuu 520 na kati ya hizo, 300 zitaanza kujengwa Machi mwaka huu.
“Mkakati wetu ni kuharakisha ujenzi wa mji huu wa kisasa ili wananchi waishi maisha watakayo kwa gharama nafuu za nyumba,” alisema.
Alisema katika nyumba hizo 300, nyumba 200 zitajengwa na NHC na 100 zitajengwa na Watumishi Housing Company kwa ajili ya watumishi wa umma.
“Tunawaomba wadau wengine wa ujenzi kushirikiana nasi katika ujenzi wa mji mpya ili kuleta mageuzi ya taswira ya mji wa Arusha,” alisema
Akifafanua, alisema kuwa nyumba zitakazojengwa na Watumishi Housing Company kwa ajili ya watumishi wa umma, zitakuwa za ghamara nafuu ili kuwawezesha wengi kumudu kuishi.
Alisema kuwa, uwapo wa nyumba hizo utasaidia kuongeza ajira kwa vijana, kwani wengi watahusika katika shughuli za ujenzi.
“Kupitia ujenzi huu wa mji mdogo, kutasaidia kurahisisha maendeleo katika maeneo haya, kwani kutakuwapo na huduma mbalimbali za kijamii,” alisema Kisarika.
Ili kufikia malengo hayo ya ujenzi, aliwataka wadau kushirikiana kufanya mageuzi ya makazi bora mkoani Arusha

No comments:

Post a Comment